.

Unavyoweza Kujiajiri Kwa Kuuza Miche Ya Miti...!


Na: Meshack Maganga- Iringa



Ndugu zangu, Wito wangu sikuzote umekuwa ni kutumia muda wangu mwingi kuwasisitiza rafikizangu, ndugu na wadau wengine wote, kuangalia uwezekano wa kuzitambua fursa mbalimbali zilizopo kwenye mazingira yetu. Hakuna sehemu yeyote ya dunia ambayo haina fursa na ambayo imesahaulika, bila kuwa na fursa za kuitosha jamii, isipokuwa macho yetu ya
ndani hayazioni fursa hizi. Vitakubwa tuliyonayo ni ya kupambana katika kuondoa mitazamo hasi iliyomo kwenye vichwa vyetu tuweze kuziona fursa hizo.

Tumezungukwa na fursa (Neema ya Mungu) ni ajabu kumsikia mtu anaeishi Morogoro ama Iringa halafu hafahamu kilimo cha vitunguu, hafahamu kama kuna kilimo cha mitiki, ama haamini kwamba kuna watu wameshafikia kwenye kilele cha mafanikio kwa kujishughulisha na kilimo cha matembele, ufugaji wa samaki na mambo mengine madogomadogo ambayo waliopitapita vyuoni wanadia kwamba ni hizo ni kazi za watu duni waliokimbia ‘umande’. 
Mtu anaishi Dar hana taarifa kwamba Bagamoyo ama Mkuranga, kuna kilimo cha mitiki, Vitunguu, nyanya, mihogo nk. Ajabu yingine kuna wanaoishi Iringa, lakini hajawahi kujifunza kilimo cha miti angalau wapande hata nusu ekari ya miti na huyu bado atakuwa anaitupia serkali lawama kwamba haimjali, swali, unataka serkali ikujali wakati unalala na kushinda facebook kupiga majungu? Badilisha mtazamo wako.

Watalaamu wa Elimu ya utambuzi na mawazo ya kina kama akina Paul Msatu wanasema kwamba, Sisi sote ni mawazo yetu, kuishi kwetu ni mawazo yetu, mafanikio yetu ni mawazo yetu, uchumi wa taifa letu ni mawazo yetu.Utamaduni wa taifa letu ni mawazo yetu. Ukweli wa maisha yetu, mafanikio yetu, upo ndani yetu katika mawazo yetu. Uwezo mkubwa unaotutofautisha kati yetu sisi na viumbe wengine upo katika mawazo yetu. Tabia zetu, matendo yetu, kuamini kwetu na zaidi kuishi kwetu ni kuwaza kwetu. Mafanikio yote duniani, utajiri wote duniani na hata umaskini wa mwanadamu vyote vimeanzia katika mawazo na mitazamo yake juu ya maisha.
Hakuna mtanzania asiyefahamu matumizi ya miti, labda kwa kukumbushana tu, baadhi ya matumizi ya miti ni kama vile, mbao, nguzo, chakula, kilimo mseto, hifadhi ya vyanzo vya maji, kurutubisha udongo, kulisha mifugo, kuboresha hali ya hewa, kuni, mkaa, dawa na mapambo.
Kosa tunalolifanya na kusababisha tuzipoteze fursa za mafanikio, hata kama zinachukua muda mrefu ni mtazamo mbaya wa kufikiri kwamba fursa za mafanikio zipo nje ya maeneo tunayoishi. Ifahamike kwamba, fursa za mafanikio ya kiroho na kimwili hutafutwa kwasababu haziwezi kujileta kwasababu zina tabia ya kujificha. Baadhi ya fursa hujileta zenyewe kwetu na kama haziji upande wetu ni vizuri tukazifuata kwenye maeneo yanayotuzunguka.
Kuna watanzania ambao wanafikiri upandaji wa miti ya mbao na nguzo ni mkoani Iringa pekee, ninapenda kutoa wito kwa watanzania wenzangu kwamba unaweza kupanda miti popote pale ulipo, (Tanzania Tree Seed Agency- TTSA) wametoa mwongozo wa upandaji miti kwa kila kanda, na kila mkoa, hakuna mkoa Tanzania ambao hakuna miti. Ukiwa Mwanza, Singida, Mbeya ama Kigoma na kwingineko panda miti inayostawi eneo hilo na faida yake utaiona. Faida ya miti huonekana baada ya miaka mingi 8-10 na kama huwezi kusubiri miaka hiyo ni bora ufanye jambo jingine.
Ili kupata faida za miti hakuna budi kufanya uchaguzi sahihi wa miti ya kupanda kwa ajili ya matumizi yaliyokusudiwa. Mfano miti inayofaa kwa kivuli ipandwe sahemu zinazohitajika kuwa na kivuli na iwe ni ile isiyopukutisha majani yote msimu wa kiangazi, miti ya kilimo mseto iwe ni miti yenye mizizi inayokwenda chini zaidi ya sentimeta 50 na iwe inayorutubisha ardhi, yenye kivuli chepesi na inayofaa kwa malisho. Miti ya mapambo iwe na maua ya kuvutia, isiwe na mizizi inayotambaa mbali na isiwe inapukutisha majani yote wakati wa kiangazi.

Hakikisha kuwa unapata mbegu bora za miti kwa ajili ya kuzalisha miche ya kutosha kupanda katika maeneo utakayoyaandaa. Mbegu hizi bora za miti zinapatikana kutoka Wakala wa Mbegu bora za miti (Tanzania Tree Seed Agency- TTSA). Ni Wakala wa Serikali ya Tanzania ambao ni idara iliyo chini ya Wizara ya Mliasili na Utalii. TTSA ina uzoefu katika takinolojia ya mbegu bora na safi za miti. Wakala pia unatoa mafunzo ya muda mfupi (majuma 2) yanayohusu uvunaji mbegu hasa kwa wale ambao hawawezi kununua mbegu kutoka TTSA, Wakala wa mbegu.

Kitalu hujengewa banda ili kuwe na kivuli kwa mbegu zinazoota. Kibanda kinaweza kuwa cha majani au fito zenye kipenyo cha sm 2 yaliyoshonwa kwa kamba kiasi cha meta 2 juu ya kitalu kwa kukiegemeza kwenye nguzo zilizofungwa pamoja na fito. Pande zote za kitalu ziachwe wazi ili hewa ipite kwa urahisi.

Inapendekezwa na baadhi ya watalamu wa kilimo cha miti kuwa - wakati miche michanga imeanza kuota majani ya kwanza, yango’lewe kwenye vitalu na ipandikizwe kwenye viriba kama ifuatavyo: kishimo kirefu zaidi kuliko mizizi ya miche kitengenezwe kwa kijiti ili mizizi isije ikapinda kuelekea juu. Pia kishimo kiwe na upana wa kutosha, vinginevyo mizizi ya pembeni itashika ukingoni na kupinda juu wakati mche ukiingizwa. 

Gharama ya kuanzisha bustani ya miche inatatofautiana kulingana na mahali bustani ilipo. Ifahamike kwamba, unaweza kuanzisha kitalu cha miche popote ulipo Tanzania, kuna wanaofikiria kwamba, uanzishaji wa kitalu cha miche lazima iwe Iringa, ama Lushoto, Morogoro ama Njombe,unachotakiwa kukifanya ni kubadilisha mtazamo. Wale wanaoishi Dar mtakuwa mmeshaona baadhi ya watanzania wenzetu pembeni mwa barabara wakiuza miti, ukiwa na akili ya kutoona mambo huwezi kuwaona. 

Ninakuhakishia popote pale ulipo unawezakuanzisha kitalu na ukauza miche, ikakuweka mjini. Kwa upande wa Iringa hasa kijiji tunachofanyia kazi sisi, gharama ya kuanzisha bustani yenye miche 100,000. Inakadiliwa kufikia shilingi milioni 4, hii inajumuisha, gharama za udongo kutoka mstuni, viriba, dawa za kuzuia wadudu, vifaa vya kujengea kitalu, mbao, misumari, vifaa vya kufanyia kazi, kama vile matoroli, mipira ya maji, watering can, majembe nk. Mbengu, na usimamizi kwa miezi mitano na banda la ofisi.
Miche huwekwa chini ya kivuli kama kile cha kitalu cha mbogamboga.na umwagiliaji wa maji hufanywa mara kwa mara kutegemea na hali ya hewa ya sehemu kitaulu kilipo.

Muda wa kupeleka miche shambani unapokaribia kivuli huondolewa polepole aidha kw kupunguza majani kwenye kibanda au kwa kuondoa kibanda kwa muda mrefu zaidi kila siku mpaka miche itapoweza kustahimili jua la moja kwa moja. Upunguzaji wa unywesheaji, dhidi ya mahitaji ya miche itumike ili “kukomaza” miche tayari kwa kupanda shambani. Viriba visogezwe mara kwa mara ili mizizi inayojitokeza chini ikatike. Njia nyingine ni kuinua viriba na kukata mzizi mkuu chini kwa kutumia kisu kikali. Viriba vinaweza kupaliliwa kwa kutumia kijiti chenye ncha kali au kutumia mkono. Miche hiyo huchuka miezi 4 na kuendelea kuikuza tangu siku ya kuipandikiza kutegemeana na miti inayohusika.

Uandaaji wa kitalu cha miche, unatakiwa ufanywe kwa makini sana, usipokuwa makini utaotesha miche isiyokuwa na tija, ukumbuke kwamba, uuzaji wa miche inaweza kuwa moja ya njia rahisi sana ya kujipatia kipato popote pale ulipo, kwa mfano, kama umeotesha kitalu cha miche 5 (elfu tano) ya mbao, kuni,dawa ama nguzo ama miti ya mapambo na kati ya hiyo miche ukabahatika kuuza miche elfu tatu kwa bei ya shilingi mia tu utakuwa na uhakika wa kuvuna shilingi laki 3, na kwanini upate laki tatu wakati unaweza kuongeza ukubwa wa ndoto yako ukapata zaidi ya laki 3? Ikumbukwe kwamba, wakati utakapokuwa unasubiri kuuza miche na pengine kuipanda kwenye mashamba yako utakuwa unajishighulisha na kazi nyinginezo kama bustani ya mboga nk. 

Maadui wakubwa wa miti ni pamoja na magonjwa, wadudu, moto na wanyama baada ya kuipanda. Adui mwingine wa kilimo cha miti ni mawazo yetu, mawazo mgando yasiyotaka kuvumilia, ukipanda mti hasa ya mbao, nguzo nk, usitegemee kuvuna baada ya mwaka mmoja, ni baada ya miaka 8 hadi kumi. Kama utaona miaka 8 ni mingi usifanye hiki kilimo hakikufai. Tafuta fursa nyingine. 

Ikumbukwe kwamba, mafanikio yanatokana na mawazo au wazo la mafanikio. Wazo linatengeneza fursa na kama utabuni wazo jipya kwenye mazingira yako utaibuka kuwa mshindi. 

Fursa za mafanikio zina gaharama yake, kuna gharama ya muda, gharama ya pesa, na kama haupo tayari kulipia hizo gharama hizo fursa zitakupita. Uchaguzi unabakia kuwa wako. “MY MOTTO IS GO BIG OR GO HOME”
Binadamu wote wenye mafanikio duniani hawachoki kutafuta..!

MAWASILIANO. meshackmaganga@gmail.com


Previous
Next Post »