.

Unachotamka Ni Matokeo Ya Mambo Yaliyopo Kichwani Mwako.


 
Na: MROPE WA MROPE. Iringa.
Tena maandiko yanasema, "yamtokayo mtu ndiyo yaliyoujaza moyo wake". Wataalamu wa lugha kama Richards&Ogden walisema  "kinachotamkwa ni kiwakilishi cha picha iliyo kichwani mwa mtu".
Wataalamu hawa waliungwa mkono na wataalamu wengine kama Edward Sapir na Nikolai Trubetzokoiy ambao nao walinogesha kwa kusema "sauti inayosikika ni
kiwakilishi cha yale yaliyo kichwani mwa mtu na kichwani ndiko kuna ukweli zaidi kuliko mdomoni".
Hawa walienda mbali na kuweka mifano kama mtu akitamka "thelathini", "selasini" "thalathini", "thalathini" msikiaji atajua kinachomaanishwa ni 30 japo uhalisia wa maneno unakataa jambo linaloashiria kuwa kilicho kichwani mwa mtu ndicho hubeba maana halisi ya mtu. Ninachotaka kusema hapa ni kuwa kile utakachoilisha akili yako ndicho kitakachoujaza moyo wako na hatimaye matamshi yako.

Swali la kujiuliza hapa, kitu gani unailisha akili yako? Stori na masimulizi yanayokujaza uoga au maelezo yanayokupa ujasiri? Hayo yaliyojaa katika akili yako ndiyo yanayokusukuma katika namna fulani ya kutenda.
Kama leo unafuatilia fulani analea mtoto ambaye hajamzaa yeye maana yake lazima uwe mtumwa wa kufuatilia hilo na likijaa kichwani mwako lazima utafute pa kulitamkia ili nafsi yako iwe na amani.
Kifupi hapo unakuwa umeajiriwa na umbea na utakuwa mtumwa wa huo umbea jambo ambalo halina faida na maisha yako. Kama akili yako imejaa mambo yasiyokuhusu utajikuta unasukumwa kutamka hayo yasiyokuhusu na watu wakitaka mjadili yanayowahusu hasa hatima ya kimaisha utaona hayana maana.
Nikuambie kuwa unahitaji sana umakini katika mambo unayoingiza kichwani mwako maana ndiyo yanayojenga maisha yako. Maisha yako yanaathiriwa na unachowaza na kutamka. Maisha yetu ni uchaguzi juu ya mambo mawili tu yaani mazuri na mabaya. Wengi watasema mimi huwa nachagua mazuri na si mabaya lakini yawezekana hayo ni mazuri kwa mujibu wa uliyoyajaza kichwani mwako na wala sio uhalisia. Teja anaona unga ni bora kuliko kuku, lakini je unga ni bora kuliko kuku? La hasha lakini ni bora kwa mujibu wa yale aliyoyajaza katika kichwa chake. Kwa mtindo huu wapo wengi sana katika maisha haya wanaochagua "unga" (madawa ya kulevya) badala ya "kuku" na wanajiona wamefanya uchaguzi sahihi katika maamuzi yao.
Unapokuja wakati wa maamuzi ndio wakati wa kufanikiwa au kuharibikiwa, kupanda au kushuka, kujenga au kubomoa na bahati mbaya muda wa maamuzi kila mtu hujiona yupo sawa ila matokeo ya maamuzi ndiyo husema ukweli. Kwa hiyo niseme mapema kuwa maamuzi yanatokana na kile tulichohifadhi katika store ya maamuzi na kama stoo ya maamuzi imejaa mambo mabaya kwako yatakuwa mazuri tu kama ilivyo kwa teja kuchagua unga.
Ninachotaka kusema ni kuwa lazima uiheshimu sana akili yako na unachokipokea katika akili yako. Tafuta maarifa ili uwe na machaguzi bora katika stoo yako ya maamuzi.
Hapa hakuna kukwepa maana mafanikio ni matokeo ya maamuzi na maamuzi ni matokeo ya uchaguzi wa yaliyo katika stoo ya kichwa chako na kinachochaguliwa toka stoo ya kichwa chako ni matokeo ya kile ulichokitafuta na kukiweka kichwani mwako. Wapi unatafuta mambo ya kuingiza kichwani mwako ambayo ndiyo huamua maisha yako???
ALOYCE MROPE, Che Mrope Wa Mrope (fb), Mbeba Maono (fb page) 0766656626/0715366010/0787641417

 
Previous
Next Post »