.

Simu Yako Unayotumia Ni Mtaji Tosha...!



Na: Albert Sanga- Iringa.
Jana nilisafiri kutoka Iringa mjini kwenda kijiji kimoja kiitwacho Ndorobo, umbali wa kilomita takribani 170(kwenda na kurudi). Hapo nilifika kuonana na kijana mjasiriamali na mpambanaji hasa; aitwaye Herry. Kijana huyu ana miaka 24; baada ya kumaliza kidato cha nne matokeo yake yalikuwa mabaya, akaamua kurisiti pia matokeo yakagoma. 

Akaona asiendelee kupoteza muda kusumbukia "vyeti vinavyogoma"; akaamua kwenda kwa
mtu kujifunza ujuzi wa kuprinti t-shirts na mabango. Alipoiva kwa ujuzi huu akachukua "muvu" ya kijasiriamali. Kwanza akazunguka katika shule mbalimbali za huko vijijini akiomba tenda ya kuprinti t-shirts na kugongesha mihuri kwenye mashati. Akapata tenda kwenye shule mojawapo(kwingine hawakuweza kumwamini mapema); changamoto ikawa ni ukosefu wa mtaji. 

Anasema alikuwa na simu yake akaamua kuiuza kwa shilingi elfu 45 kisha akaenda kununulia t-shirts chache, na materials ya kazi. Akaanza kidogo kidogo, akaanza kupata faida, sifa zake zikaenea mahali pengi; na sasa ana tenda katika vikundi vya vikoba, ma-saccoss, na mashule zaidi ya hamsini.
In short ni kwamba anavuna hela! Faida aliyoikusanya akaipeleka kwenye biashara ya mashine za kusaga na kukoboa alizonazo katika vijiji vitatu tofauti; na pia ana mashamba ya mpunga ekari nyingi.

 Na sasa anajiandaa kuagiza mtambo wa kisasa wa kuprintia na kuchapishia kutoka China. Amejenga nyumba na ana viwanja vingine vitatu Iringa mjini; yote akiwa na umri wa miaka 24 na bado anaishi zake kijijini. Kuna masomo 15 nimejifunza kutoka kwa kijana Herry, lakini hapa ngoja nikushirikishe matatu: 1) Kusoma ni kuzuri lakini kama hukubahatika kusoma ama kama akili ya darasani huna; usipoteze muda kunung'unika ama kurisiti miaka nenda rudi; jaribu mambo mengine; kwa sababu kutoka kimaisha hakupo katika kusoma pekee! 2) Suala la kudhani unashindwa kufanya biashara kwa sababu huna mtaji, hebu lifikirie upya kwa sababu hata Simu Yako Unayotumia Ni Mtaji Tosha unaoweza kukutiririshia ‘ulakionea’ na hata umilionea 3). 

Watu wengi wakishapata "vielimu" ama wanaotafuta maisha; wamekariri kwamba kutoka kimaisha kupo mjini. Uhalisia ni kwamba mjini kila mtu ni mjanja na fursa nyingi zimeshatwaliwa; wengi wapo mijini ila wanasindikiza wengine; vijijini kuna fursa nyingi na rahisi. Ni suala la ku-tune tu mtazamo wako. ~SmartMind~
Previous
Next Post »