.

BIASHARA ZINATAKA "TIMING"..!!



 Na : Albert Sanga- Iringa

Mwaka 2008 nilifunguo chuo cha mafunzo ya kompyuta(Stepwise Universal College) huko wilayani Mufindi Iringa. Mbali na mafunzo ya kompyuta na ukatibu mahsusi(Secretarial Courses), chuo kilikuwa kikifanya biashara ya kutoa huduma ya Internet(kwa mtandao wa TTCL). 

Wakati huo simu za mkononi zenye internet zilikuwa chache na gharama sana; hivyo; wateja hawakuwa na chaguo katika maeneo yale zaidi ya "kuniungisha"; ambapo lisaa limoja tulikuwa tunachaji Tsh. 5,000 (elfu tano hii unayoijua) na asikwambie mtu nilikuwa natengeneza hela kama "mvua" na
faida ilikuwa kubwa kupindukia(supernormal profit). Mwaka 2010 nikajaribu kufungua tawi mjini Makambako, nikitegemea mambo yatakwenda kama nilikoanzia; looh! Nilipofika hapo kwanza nikakuta kuna "internet cafes" nyingi pili wakawa wanachaji Tsh. 1,000 tu kwa lisaa! Faida ikapungua mara tano! Si hivo tu, punde si punde, simu za mchina zikaanza kuingia kwa fujo kiasi kwamba kupata wateja ikawa ni mara moja moja sana.

Mwaka 2011 nikajaribu kuhamishia biashara hizi Iringa mjini, ila nikagundua ni kugumu mara mia ya nilikoanzia. Baadae niliuza ile biashara yote nikaingia kwenye biashara zingine. Nimekusimulia hii ili nipate upenyo wa kukueleza mambo matatu kuhusu biashara. 1) Biashara zinabadilika kwa spidi sana, kuzalisha faida kwenye biashara (hasa nyakati hizi) unahitaji timing ya hali ya juu sana. 

Watu wamekuwa wajanja sana, wanaiga haraka na wanatafiti sana. Leo "ukiotea" biashara inayokupa faida kubwa, watu wanakupa miezi michache, wanakusoma halafu ghafla bin vuu utaona kila mtu kaanzisha biashara kama yako; usipokuwa mjanja wa kubadilika ama kuboresha; mtaanza kunyang'anyana wateja na utajikuta biashara inakuwea ngumu na hata kufa. Kilichonipata mimi ni kuwa biashara ya internet ilikuwa inabadilika halafu mimi nilibakia na mawazo ya kizamani, kutegemea faida kubwa bila ubunifu mpya! Usinicheke!! Nenda kawaulize wafanyabiashara waliotikisa kwa biashara ya vibanda vya kupigisha simu, halafu wakawa wazito wa kusoma upepo na kubadilika! 2) Unapotaka kuanzisha biashara hakikisha una taarifa halisi na za karibuni kuhusu biashara hiyo, vinginevyo utaliwa. 

Kwa kuwa ulisikia mwaka jana kuwa bodaboda zinalipa, unakimbilia leo kuchukua mkopo na kununua bodaboda kumbe hiyo biashara imeshaingiliwa na mdudu! Kwa kuwa huko nyuma ulisikia biashara ya nazi inalipa, unajichomeka kuingiza mtaji, kumbe huna habari kuwa Azam siku hizi anasindika nazi na kuuza kwenye pakiti; nazi zako zitadoda! 3) MWISHO NINAKUPA RAI: Karibu kwenye ulimwengu wa biashara na ujasiriamali; ila jiandae kiakili, huku hakuna "hit and win", kuna hitaji misuli, uvumilivu, ujanja na moyo wa chuma; uzuri ni kuwa "anaejaribu" tena na tena bila kukata tamaa ndie "ANAE-WIN" ~SmartMind~

Previous
Next Post »