.

TANZANIA HAKUNA TATIZO LA AJIRA.



Na:  Albert Sanga, Iringa 
Wakati fulani nimewahi kufanya biashara ya daladala na nilikuwa na magari kama matatu hivi. wafuatiliajI wa safu hii bila haka mnakumbuka kuwa wakati fulani huko nyuma nimewahi kuchambua kwa kina chungu na tamu za biashara za daladala. Si kuudi langu leo kuelezea ‘chungu na tamu’ za biashara za daladala, isipokuwa kunaai nimewahi kufanya biashara ya daladala na nilikuwa na magari kama matatu hivi. wale
uzoefu nataka niutohoe kutoka kwenye biashara hii kuhusu wafanyakazi.

Kwa kumiliki magari matatu niliweza kuajiri wafanyakazi saba; madereva watatu, makondakta watatu na msimamizi mmoja. Kuna mambo yanapelekesha katika biashara ya daladala, mojawapo kubwa likiwa ni wafanyakazi. Ngoja nikupe visa viwili vinavyowahusu. 

Kwa kawaida niliweka utaratibu kwamba magari yote ni lazima yawe yamepaki kabla ya saa mbili usiku na mahesabu ya siku yawe yamewasilishwa. Siku moja gari mojawapo likaonekana halijapaki kwa muda husika na dereva wala kondakta wote hawapatikani kwenye simu. Usiku ukapita, kesho ikafika gari halijaonekana wala dereva hajulikani alipo. 

Msako na upelelezi vikaanza na hatimaye nikapata taarifa kuwa gari ilikodiwa kwenda kijiji fulani umbali wa kilomita themanini kutoka Iringa mjini. Kutokana na ubovu wa barabara gari ikaharibu difu na kutoboa ‘sample(kifaa kinachotunza oili)’. Baada ya ‘sample’ kutoboka hawakutilia manani, wakaendelea kutembeza gari na hatimaye ikaua injini. Nikatoka na gari nyingine tukaenda kuivuta na baada ya hapo nikawafukuza kazi dereva na kondakta wake. 

Kisa cha pili; siku moja majira ya saa tatu usiku nikapigiwa simu, “Hallo, wewe ndie Nyaluke? (jina la biashara kwenye magari nilikuwa nikitumia Nyaluke Trans)” Baada ya kujibu akanipa taarifa, “Gari lako lipo hapa limegonga mtu na kisha limegonga nyumba ya watu hivyo fika haraka”. Nikatoka mbio mbio kwenda eneo la tukio na nikajionea ajali ambayo ilikuwa kama sinema vile.
Kumbe dereva baada ya kukabidhi hesabu akachukua gari na kudai anakwenda kuliosha, badala yake akaingia kunywa pombe. Akiwa amelewa, wakati anarudisha gari kwa kupaki akagonga gari nyingine. Badala ya kusimama akaanza kukimbia na gari, katika kukimbia akagonga mtu, na akaendelea kukimbia ndipo hatimaye akagonga nyumba na yeye akakimbia. Huyu naye akaniachia hasara kubwa, gari likiwa limechakaa nyang’anyang’a. Dereva alikutana na mkono wa sheria lakini hilo halikuweza kufidia hasara kwa upande wangu.

Baadae nikaona hasara zimezidi nikaamua kukata bima kubwa za magari yote; lakini hilo halikuwa mwarobaini. Matatizo mengine yakaendelea kubaki ambayo kimsingi ndio kichefuchefu kikubwa katika biashara ya daladala. Ugomvi na wafanyakazi ukawa kwenye hesabu. Leo wanakuletea hesabu pungufu kisa biashara ilikuwa mbaya. 

Kesho wakitaka kukuibia; wanapiga ruti na wanapata hela za kuwatosha; kisha wanapeleka gari gereji, ‘wakizuga’ kuwa liliharibika! Na wakishaingia gereji ujue hesabu ya jioni itakuwa ni hadithi. Acha hilo, kuna siku wanajisikia tu na hawaamshi gari, achilia mbali makosa wanayofanya barabarani kiuzembe ambayo yanapelekea faini za ‘kutosha’.





Fukuza fukuza ya wafanyakazi, kuelimisha, kupangiana mikakati, kupelekana polisi; vyote hivyo nilikuwa nikihangaika navyo, lakini mambo bado yalikuwa pasua kichwa. Kuna saa nilikuwa nabahatika kupata madereva wazuri, lakini changamoto za wafanyakazi ‘vimeo’ zilizidi ‘unga’.
Baadae niliamua kuachana na biashara hii na kuingia kwenye biashara zingine. Simaanishi kwamba biashara ya daladala haina faida, la hasha! Faida ipo na mimi nilitengeneza faida kwa kiasi chache. Ninachotaka ukione hapa ni kuwa ugumu ama changamoto katika biashara hii unachangiwa pia na hulka waliyonayo wafanyakazi.

Ili uweze kuzalisha biashara ya daladala inabidi uwe ‘ngumi mkononi’ yaani uwe mkali. Ukiwa wa kucheka cheka na madereva na makonda, utavuna mabua, kwa maana utafika wakati utajikuta gari limechakaa na fedha huna. Nini maana yake? Maana yake ni kwamba kuna mushkeli upo kwenye mitazamo, tabia na uaminifu katikati ya wafanyakazi walio wengi (sio wote) katika eneo hili.
Wafanyakazi vimeo katika maeneo mbalimbali wamekuwa sababu ya biashara nyingi kufa, kupata hasara ama hata kufungwa na wamiliki. Si hivyo tu lakini wapo watu wenye kiu ya kuanzisha biashara lakini kila wakifikiria “nitapata wapi wafanyakazi waaminifu?” wanaahirisha kufungua biashara zilizomo vichwani mwao.

Mathalani, kwa mimi kupoteza magari mawili kwa uzembe wa wafanyakazi maana yake, ajira nne zilipotea. Kwa kuamua kuachana kabisa na biashara hiyo maana yake kuna ajira saba zilipotea. Je, ni watu wangapi ambao wanaamua kufunga ama kutoanzisha kabisa biashara kutokana na tatizo la wafanyakazi waaminifu?

Mara nyingi kilio cha ukosefu wa ajira kwa Tanzania tumekiweka kisiasa mno na tunakwepa uhalisia. Je, ni watanzania wangapi ambao unapowapatia kazi hufanya kwa uaminifu na kwa ufanisi? Ukitaka kufahamu hili, jaribu kuwatafuta wafanyabiashara wa maduka (makubwa na madogo) watakueleza changamoto wanazopata kwa wafanyakazi wa kuuza maduka. 

Wamiliki wengi wa maduka wanalia uhaba wa vijana waaminifu kwa ajili ya kuendesha(kuuza) maduka yao. Hii ina maana wapo ambao huamua kufunga kabisa maduka yao, wapo ambao licha ya kuwa wana mitaji lakini hawawezi kuanzisha maduka kutokana na ‘kukosekana kwa wafanyakazi’. Vile vile wapo ambao wangeweza kufungua matawi ya biashara zao, lakini wakifikiria “taabu” wanayopata kutoka kwa wafanyakazi waliopo wanakata tamaa kabisa ya kufungua matawi mengine.
Kuna matatizo matatu ambayo yanaliandama soko la ajira Tanzania. Mosi, ni uwezo wa watafuta ajira, pili ni tabia za watafuta ajira na tatu ni maono ya watafuta ajira. Kuanzia watafuta ajira wenye elimu kubwa, ya kati mpaka wale wasio na elimu kabisa.

Leo hii mtafuta ajira anapotafuta ajira kichwani mwake anawaza kutajirika ndani ya muda mfupi. Vijana wasomi leo wanapotafuta ajira wanafikiria ‘ghafla bin vuu’ wapate magari ‘makali’ wapate nyumba ‘zenye hadhi ya uhekalu’ na pia wawe na maisha kama ya ‘mamtoni’. Wenye elimu ndogo nao wana maono yao hatari kwa taasisi na biashara wanazoajiriwa. 

Tupo kwenye hali mbaya kwa sababu hata ukimuajiri kijana wa kukutunzia ng’ombe nae anawaza ‘kutoka kimaisha’ kwa kukuibia maziwa! Watafute wafugaji watakuambia namna wafanyakazi walivyo pasua kichwa. Ukimuajiri muuza duka anaiba hadi mtaji kwa sababu nae anataka awe na maisha mazuri ‘haraka haraka’. Haya ni maono hafifu na yanatengeneza roho ya wizi kabla hata ajira haijapatikana

Uwezo wa kiutendaji nao umekuwa ni tatizo kubwa. Nadhani hili limeanzia kwenye mifumo yetu ya kielimu na utamaduni. Tumekuwa na mifumo ya elimu (kutoka chini mpaka vyuo vikuu) ambayo inatia msisitizo katika nadharia na mitihani kuliko ujuzi na utendaji. 

Si jambo la ajabu kukutana na msomi, injinia, wa “Computer Software Production” ambaye hana uwezo wa kutengeneza hizo “softawares” licha ya kwamba cheti kinaonesha kafaulu vizuri. Mtu ambae ana vyeti lakini hana uwezo aajiriwe kwa lipi? 

Lakini pia watanzania wengi hatuna utamaduni wa kufanya kazi kwa bidii na kwa kukimbizana. Wengi tuna ‘kauvivu’ fulani kuanzia katika shughuli zetu binafsi. Unamuajiri mtu kwa mategemeo makubwa lakini unakuja kusikitishwa na ufanyaji kazi wake. Uvivu huu umo katika kufikiri na kutenda ndio maana licha ya kwamba nchi hii imefurika fursa, lakini wengi ‘wamezuia’ fikra zao zisione na hivyo wanaishia kuwa “walalamishi”.

Wako wapi watanzania ambao ukiwaajiri leo wanaweza kufanya kazi hizo kama za kwao? Katika ajira nyingi za umma (hasa serikalini), hulka za wengi (wanaoajiriwa) ni kutochukulia kwa umakini ajira zao. Lakini ni vema kufahamu kuwa sekta binafsi ndio inayochukua hatamu za soko la ajira kwa sasa. Huwezi kuleta ‘ujanja ujanja’ katika sekta binafsi halafu ukategemea kubaki na ajira yako.

Hali ya soko la ajira, tabia na mienendo ya wafanyakazi watarajiwa ilivyo inanifanya nijiridhishe kwamba nchi hii haina tatizo la ajira, isipokuwa ina tatizo la “kutokuwepo na wafanyakazi wa kutosha”. Hata katika sekta binafsi, kilio cha ukosefu wa mitaji hakina mashiko (nimepata kulichambua hili mara nyingi); isipokuwa kuna ukosefu wa maono, bidii, kujituma na fikra sahihi.
Badala ya kumwaga fedha kwa tunaotaka wajiajiri, huu ni wakati mzuri wa kuwamwagia maono na kuwajengea fikra. Ukimpa masikini fedha ujue unamuua, ila ukimpa maono huna sababu ya kumpa fedha kwa sababu ataweza kujitafutia mtaji. Ikiwa “watafuta ajira” watakuwa na maono, ninathibitisha pasipo shaka ya kwamba nchi hii ina ajira nyingi kuliko idadi ya wananchi wote pamoja na watoto watakaozaliwa kesho!

Wiki iliyopita nilibainisha kuwa nitaanza safari za mikoani kuzungumza na kubadilishana mawazo na wafanyabiashara, wafanyakazi(kutoka taasisi mbalimbali za umma na binafsi), vikundi vya kiuchumi, wanavyuo, na watu binafsi; kwa lengo la kushirikishana fursa, uzoefu wa biashara na mbinu zingine za kiuchumi. 

Katika mialiko niliyopokea kwa kwa awamu ya kwanza nitafika Lindi, Dodoma na Dar es Salaam. Ninashukuru kwamba wapo ambao wameendelea kunialika. Ndugu mmoja kutoka Mwanza amenipa mwaliko na nitazungumza katika semina ya kiuchumi inayoendelea kuandaliwa. Iwe ni taasisi, kikundi ama mtu mmoja mmoja; ikiwa utatamani nifike/nipitie kwa ajili ya maarifa ya kiuchumi na kibiashara, wasiliana nami mapema kwa ajili ya kuingiza kwenye ratiba. 

Kumbuka kuwa lengo kubwa mwaka huu ni: “Kutengeneza wafanyabiashara wapya, na kuinua viwango vya wale ambao tayari wapo katika biashara”. Hivyo ziara zangu mikoani ni sehemu ya utekelezaji wa lengo hili ili kuipa maana na thamani zaidi safu hii. Unaweza kuwasiliana nami moja kwa moja ama kupitia kwa Mratibu Mtendaji wa ziara hizi Bw. Jonas, 0788 155010
Wasalaam!
0719 127 901, tepwiseexpert@gmail.com




Previous
Next Post »